MWANZA YAVUNJA REKODI YA MAUAJI YA WIVU WA MAPENZI
IKIWA ni siku chache baada ya mkazi wa 
Mtaa wa Kanyerere jijini Mwanza, Maximilian Ndegere (40) Mwanza kumuua 
mkewe Teddy Patrick (38) kwa risasi na kisha yeye kujiua, matukio ya 
wanandoa kuuana kutokana na migogoro ya kifamilia na wivu wa kimapenzi 
yameendelea kutokea jijini Mwanza.
Kutokana na mauaji hayo, Jeshi la Polisi
 jijini Mwanza linamsaka kwa udi na uvumba mwanamume ambaye amemuua 
mkewe kwa kile kinachoonekana kuwa ni wivu wa mapenzi na kisha kutokomea
 kusikojulikana.
Akizungumza na waandishi wa habari 
jijini hapa jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Ahmed Msangi alisema polisi
 wanamtafuta Charles John (35) ambaye ni mkazi wa Pasiansi Mashariki 
katika Kata ya Pasiansi, Manispaa ya Ilemela.
Kamanda Msangi alisema John alishiriki 
katika tukio la kumpiga mkewe Ester Charles (30), Mei 30 mwaka huu saa 
9.09 alfajiri na kumwacha akiwa amekufa chumbani kwake huku mwili ukiwa 
na majeraha.
Alisema katika kipindi chote cha 
mahusiano yao, wawili hao walikuwa kwenye migogoro ya mara kwa mara ya 
kifamilia, ambayo mwanamke huyo alikuwa akimtuhumu mumewe kuwa na 
uhusiano wa kimapenzi na mwanamke mwingine.
Alisema siku hiyo ya ugomvi, majirani 
walisikia ugomvi ukiendelea kati ya wanandoa hao, na walikwenda 
kuwasuluhisha na kuwasaidia kwa vile walizoea kuwasikia wakipigana mara 
kwa mara na kisha kuelewana na kuendelea na maisha yao kama kawaida.
“Baada ya muda kupita majirani 
hawakusikia ugomvi tena, na kudhani kuwa wameelewana, lakini baadaye 
alisikika mtoto mdogo akilia kwa muda mrefu ndipo majirani walikwenda 
dirishani kuangalia na kumuona mama yake akiwa amelala kimya kitandani 
bila ya kumsaidia mtoto, huku baba yake akiwa hayupo, walipata shaka na 
kutoa taarifa polisi,” alifafanua Kamanda Msangi.
Alisema baada ya polisi kupata taarifa 
walikwenda kwenye eneo la tukio na kumkuta Ester akiwa tayari amekufa 
huku mwili wake ukiwa na majeraha ya kupigwa na kitu kizito. Aidha 
shingo yake ilikuwa imekabwa na kitambaa kigumu.
“Baada ya mume, kuona mke wake amekufa, 
huyu aliamua kukimbia kusikojulikana na sisi tumeanzisha msako mkali wa 
kumtafuta na tutahakikisha tunamkamata,” alieleza.
Alisema polisi inaendelea na uchunguzi 
wa mauaji hayo ya kinyama na kuongeza kuwa mwili wa marehemu 
umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando kwa ajili ya uchunguzi
 na uchunguzi utakapokamilika utakabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa 
ajili ya maziko.
Katika tukio jingine, Kamanda Msangi 
alisema Melikiad Misana (50) ambaye ni mkazi wa Miriti wilayani Ukerewe 
amekufa wakati akiwa njiani kukimbizwa hospitalini baada ya kuchomwa na 
kitu chenye ncha kali mgongoni kwake upande wa kushoto na mkewe 
Bukherehere William (25) ambaye naye alijeruhiwa na mumewe kwa kuchomwa 
na kitu chenye ncha kali kwenye mikono yake, tumboni na kusababisha 
utumbo kutoka nje baada ya kuzuka kwa ugomvi baina yao.
Kamanda Msangi alisema uhalifu huo 
ulifanyika Mei 29, mwaka huu saa 4.15 asubuhi katika Kitongoji cha 
Kamengo Kijiji cha Muriti Tarafa ya Ilangara wilayani Ukerewe, ambako 
inadaiwa siku ya tukio, Bukherehere hakulala nyumbani kwake, lakini 
baadaye alirudi nyumbani akiwa amelewa chakari kitendo ambacho 
hakikumfurahisha mkewe.
“Kutokana na hali hiyo, wanandoa hao 
walijikuta wakiingia kwenye ugomvi na kisha kuanza kupigana kwa kutumia 
vitu vyenye ncha kali, huku kila mmoja akimchoma mwenzake hali 
iliyosababisha wote kupoteza fahamu kutokana na majeraha waliyopata,” 
alifafanua Kamanda Msangi.
Alisema baada ya majirani kupata 
taarifa, walitoa taarifa polisi na polisi walipofika kwenye eneo la 
tukio waliwachukua majeruhi na kuwakimbiza hospitalini, lakini wakiwa 
njiani mwanamume alifariki dunia huku mkewe akiwa hajitambui.
Alisema majeruhi amelazwa katika 
Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe akiendelea kupatiwa matibabu akiwa chini 
ya ulinzi wa polisi huku polisi wakiendelea na upelelezi kuhusu mauaji 
hayo. Alisema hali yake sio nzuri na mwili wa mumewe umehifadhiwa 
hospitalini hapo kwa ajili ya uchunguzi
.
IMEANDIKWA NA NASHON KENNEDY,-HABARILEO MWANZA
No comments