Magufuli: Majambazi lazima watakamatwa hawatapenya.
RAIS John Magufuli amesema kundi la 
majambazi linaloendesha mauaji mkoani Pwani hasa katika wilaya za 
Mkuranga na Kibiti halitapenya, bali litakamatwa kokote waliko.
Amesema
 amani ni jambo la msingi katika uwekezaji na akawataka wananchi 
kuwaambia ndugu zao ambao wanawafahamu kwamba wanafanya vitendo hivyo, 
kuacha mara moja.
“Hawatapenya, vyombo
 vya ulinzi na usalama viko imara, hapo walikuwa wanajaribu kupiga mruzi
 tu,” alisema Rais Magufuli jana asubuhi alipozungumza na wananchi wa 
Kijiji cha Mkiu Wilaya ya Mkuranga wakati wa kuweka jiwe la msingi la 
Kiwanda cha Vigae cha Good Will.
Alisema nchi inahitaji amani ili wawekezaji waje kwa wingi, kuwekeza miradi mbalimbali.
Alisema
 Mkoa wa Pwani umebadilika kutokana na viwanda vingi kujengwa mkoani 
humo na kusaidia kupunguza tatizo la ajira. “Wilaya ya Mkuranga peke 
yake ina viwanda 83, naambiwa Mkoa wa Pwani una viwanda zaidi ya 200, 
haya ndio maendeleo tunayotaka, akitokea mtu anahatarisha uwekezaji huu 
lazima tushughulike naye,” alisema Rais Magufuli.
Aliwahakikishia
 wawekezaji wa kiwanda hicho cha GoodWill Tanzania Ceramic Co. Ltd kuwa 
amani itakuwepo eneo hilo na wasifikirie kwenda kujenga viwanda vingine 
nje ya Tanzania, bali waendelee kujenga viwanda vingine vingi katika 
wilaya hiyo.
“Jengeni hapa viwanda 
vingi, bahati nzuri sisi ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na 
SADC, soko la ukanda huu ni kama watu milioni 500, hivyo kuna uhakika wa
 soko la bidhaa zenu, hivyo jengeni viwanda vingi hadi huko baharini,” 
alisema Rais Magufuli.
Kiwanda cha 
Vigae cha Good- Will kinatumia gesi asilia na asilimia 95 ya malighafi 
ya kiwanda hicho, inapatikana eneo hilo na asilimia tano tu ndio 
inayoagizwa kutoka China.
Kina uwezo 
wa kuajiri watu kati ya 1,000 na 1,500. Katika hatua nyingine, Rais 
Magufuli amesisitiza kwamba kama kuna wananchi wanasubiri chakula cha 
bure kupelekewa na serikali, watakufa kwa njaa kwani hakuna vya bure 
chini ya utawala wake.
“Hizi kauli 
zilizokuwa zinatolewa huko nyuma eti hakuna mwananchi atakayekufa kwa 
njaa, mimi siiungi mkono. Sasa nasema chini ya utawala wangu kuna watu 
watakufa kwa njaa wasipofanya kazi. Lazima tuambiane ukweli,” alisema 
Rais Magufuli.

No comments